SAID JUMA IRANDO2  
Dar es Salaam. Mwanafunzi bora wa kwanza kitaifa katika matokeo 
yaliyorekebishwa ya mtihani wa kidato cha nne uliofanyika mwaka 2012, 
Said Irando kutoka Shule ya Sekondari Feza ya jijini Dar es Salaam, 
ameeleza kushangazwa na matokeo hayo kwa kuwa hakuyatarajia.
                
              
Mwanafunzi huyo ambaye tayari ameshaanza masomo ya
 Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari Feza, alisema kuwa ingawa 
alisoma kwa bidii lakini hakudhani kama angeweza kushika nafasi ya 
kwanza kitaifa na kwamba anamini mafanikio yake kitaaluma yana ‘mkono wa
 Mungu’.
                
              
“Sikutegemea kabisa kuwa mwanafunzi bora, ingawa 
nilisoma kwa bidii kubwa nia yangu ilikuwa ni kutaka kufaulu tu; Ni 
Mungu amenisaidia,” alisema Irando.
                
              
Alisema kujituma katika masomo, mazingira mazuri 
ya kusomea na upatikanaji wa vifaa muhimu vya kujifunzia ndiyo 
yaliyomwezesha kusoma na kufanya vizuri.
                
              
Irando ambaye ni mtoto wa kwanza katika familia 
yenye watoto watatu, alisema kurekebishwa kwa matokeo ya kidato cha nne 
kulibadilisha alama za matokeo yake kutoka Daraja la kwanza akiwa na 
alama tisa hadi saba, zilizomfanya kuwa mwanafunzi bora kitaifa na 
mwafunzi bora wa kwanza kati ya wavulana kumi bora pia kitaifa.
                
              
Mwanafunzi huyo alibainisha kuwa pamoja na wazazi 
wake kuwa ni wafanyabiashara, yeye anatamani kuwa mhandisi ingawa bado 
hajajua atakuwa mhandisi katika tasnia gani.
                
              
“Natamani sana kuwa mhandisi hiyo ndiyo ndoto yangu ingawa bado sijajua nitakuwa mhandisi wa sekta gani,” alisema Irando.
                
              
Irando alisoma elimu ya msingi katika Shule ya 
Msingi J.K Nyerere ambako alifaulu na kuchaguliwa kujiunga na Sekondari 
Pugu, lakini wazazi wake waliamua kumpeleka Shule ya Sekondari Feza.
                
              
Naye mwanafunzi Joshua Azza kutoka Sekondari ya 
Wavulana Marian ambaye ameshika nafasi ya saba kitaifa kati ya wanafunzi
 kumi bora baada ya kupata daraja la kwanza akiwa na alama 11, alisema 
ameyapokea matokeo hayo kwa furaha akiamini atatimiza lengo lake la kuwa
 daktari wa upasuaji.
                
              
“Natarajia kuwa daktari wa upasuaji, kwa matokeo 
haya nadhani nitafanikiwa,” alisema Azza ambaye wazazi wake wote ni 
walimu alipozungumza na gazeti hili jana jijini Dar es Salaam.
                
              
Kwa upande wake Saidi Nchimbi kutoka Sekondari ya 
Feza, ambaye ameshika nafasi ya nane kati ya wanafunzi kumi bora 
kitaifa, alisema kuwa siku zote alikuwa akisoma kwa uwezo wake wote na 
kwamba alikuwa akitamani kufaulu kwenye mitihani yake yote aliyopewa.
                
              
Nchimbi amefanikiwa kushika nafasi hiyo baada ya 
kupata daraja la kwanza akiwa na alama nane. Katika matokeo ya awali 
mwanafunzi huyo alikuwa na alama 11.
 
